wavuti.com Updates

-------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Napenda kuwataarifu kuwa blogu hii inapumzishwa rasmi na tovuti mpya imezaliwa kwa jina www.wavuti.com

This is to inform you that this blog has been retired. A new website to take her place is up and running at www.wavuti.com

Thursday, October 08, 2009

TweetThis! Taarifa kwa vyombo vya habari kuhusu afya ya Raisi wa Tanzania

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

Telephone: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: press@ikulu.go.tz
Fax: 255-22-2113425

PRESIDENT’S OFFICE,
THE STATE HOUSE,
P.O. BOX 9120,
DAR ES SALAAM.
Tanzania.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mimi naitwa Dk. Peter Mfisi, ni mmoja wa madaktari wa Mhe. Rais. Nipo Ikulu. Nimekuwa na Mhe. Rais tangu wakati wa kampeni mwaka 2005 mpaka sasa. Mwenzangu ni Dk. Mohamedi Janabi ambaye ni daktari bingwa wa maradhi ya moyo katika Hospitali Kuu ya Taifa Muhimbili.

Nimewaiteni waandishi wa habari kufafanua masuala muhimu kuhusu afya ya Mhe. Rais kufuatia tukio la Jumapili iliyopita, Oktoba 4, 2009, pale Mwanza.

Tukio hilo limeleta mshtuko kwa watu wengi na kuendelea kuwa jambo linalozua mjadala kuhusu hali ya afya ya Mhe. Rais. Naelewa sababu ya wananchi kuwa na hofu na kuwapo kwa mjadala miongoni mwao. Rais ndiyo kiongozi wetu mkuu katika taifa na hivyo kuwa mwenye afya njema ndiyo matakwa ya kila mwananchi.

Naelewa fika kuwa kutokana na kiapo changu cha udaktari na maadili yangu ya kazi siruhusiwi kutoa hadharani undani wa habari yoyote inayohusu mgonjwa ninayemtibu bila ridhaa yake.

Hata hivyo, kwa kuwa huyo ni Rais wa nchi, na suala la afya yake ni kwa maslahi ya taifa na umma wa Watanzania kwa jumla, na kwa kuwa yeye ameridhia kutolewa kwa habari za afya yake ili watu wajue ukweli na kuondoa hofu, nimeamua kufanya hivyo.

Kama sote tujuavyo, Jumapili iliyopita, Oktoba 4, 2009 mwaka huu, Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa anashiriki katika sherehe za miaka 100 ya Kanisa la Africa Inland Church Tanzania (AICT) kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, aliishiwa nguvu na kulazimika kwenda kwenye chumba cha mapumziko.

Baada ya mapumziko ya dakika 10 hivi, Mhe. Rais alirejea kwenye shughuli hiyo na kuendelea kushirikiana na waumini wa AICT hadi mwisho wa ratiba yake.

Ninapenda kusisitiza kuwa tukio la Mwanza limetokana na Mhe. Rais kuzidiwa na uchovu, na wala siyo kwa sababu nyingine yoyote ya kiafya. Wakati tukio hilo linatokea nilikuwepo, nilichukua vipimo muhimu kama daktari anavyotakiwa kufanya linapotokea tukio kama lile kwa mtu. Vipimo vyote vilithibitisha kuwa Mhe. Rais hakuwa na matatizo yoyote ya kiafya ambayo yangeweza kuhusishwa kuwa chanzo cha tukio lile.

Pressure yake ilikuwa 130/85mmhg ambayo ni kiwango cha kawaida kwa mtu wa umri wake. Mapigo ya moyo wake yalikuwa 76 kwa dakika ambayo pia ni ya kawaida. Sukari kwenye damu ilikuwa 5.5mmol/l ambayo nayo ilikuwa ya kiwango cha kawaida. Joto la mwili lilikuwa digrii 37.5 centigrade ambalo ni la kawaida. Mhe. Rais pia hakuwa na kiungo chochote kilichoonekana kutetereka, jambo ambalo lilithibitisha kuwa hakupata kiharusi.

Kutokana na matokeo hayo, sikuona hatari yoyote ya yeye kuendelea kushiriki katika sherehe hiyo muhimu kwa wakati huo. Ndiyo maana niliruhusu aendelee kushiriki sherehe zile mpaka alipomaliza na kuondoka.

Baada ya kurudi Dar es Salaam siku ile niliwasiliana na madaktari wanzangu wa hapa nchini na nje ya nchi ambao tumekuwa tunashirikiana nao katika kuchunguza na kufuatilia afya ya Mhe. Rais. Wote hao baada ya kuwasimulia kilichotokea na matokeo ya vipimo nilivyomfanyia Mhe. Rais, kwa tafakuri zao hawakuwa na wasiwasi wowote kuwa tukio hilo lilisababishwa na jambo jingine lolote, isipokuwa uchovu. Imani yao inatokana na ukweli kuwa wanaifahamu vizuri hali ya afya ya Mhe. Rais kwa kuwa wanahusika katika kuifuatilia mara kwa mara. Mmoja wao alimuona Mhe. Rais siku moja kabla ya kuondoka New York ambapo alipata nafasi ya kuchunguza afya yake.

Mimi na mwenzangu Dk. Mohammed Janabi, ndiyo wenye dhamana ya kuiangalia afya ya Mhe. Rais Kikwete kila siku. Tumekuwa tunafanya hivyo kwa zamu na wakati mwingine kwa pamoja, inapobidi kufanya hivyo. Katika kufuatilia hali ya afya ya Mhe. Rais tumekuwa pia tukimfanyia uchunguzi wa afya yake kwa vipindi maalum hapa nchini na nje ya nchi kwa vipimo ambavyo hapa nchini havipo. Napenda kuwahakikishia wananchi wenzagu kuwa katika miaka hii minne Mhe. Rais wetu amefanyiwa uchunguzi wa kina wa afya yake. Nadiriki kusema kuwa hakuna kipimo ambacho hatujapata kukifanya katika uchunguzi wa mambo muhimu ya afya yake.

Kwa sababu ya kuwatoa hofu wananchi na kwa vile mwenyewe anaridhia tufanye hivyo napenda kuwapa ufafanuzi kuhusu hali ya afya ya Mhe. Rais. Katika hali ya kawaida nisingefanya hivyo kwa sababu maadili ya kazi ya udaktari yanakataza. Naamini madaktari wenzangu wataelewa mazingira niliyokuwa nayo. Katika kufuatilia afya ya rais tumekuwa tunaangalia na kuchunguza mambo yafuatayo.

(a)Blood Pressure: Tunafuatilia kwa karibu sana hali ya nguvu ya msukumo wa damu (blood pressure). Tunampima mara kwa mara na mwenyewe tumempa mashine ya kujipima kila siku na anafanya hivyo. Kwa jumla pressure yake iko kwenye viwango vya kawaida. Aidha, uzito wake wa mwili unaendena ipasavyo na urefu wake. Mhe. Rais ni mtu mwenye mazoea ya kufanya mazoezi na yuko makini katika chakula anachokula. Sisi tunahusika kwa ukamilifu na kuelekeza kuhusu chakula anachokula. Hatuna matatuzi na Mhe. Rais kwa jambo hilo. Ana nidhamu ya kujipima pamoja na mazoezi na chakula.

(b)Moyo: Tumekuwa tunafuatilia kwa karibu hali ya afya ya moyo wake. Tumemfanyia vipimo kama vya ECHO, ECG na vinginevyo, na hatujabaini kuwepo tatizo lolote.

(c)Ubongo: Mwaka uliopita, 2008, Mhe. Rais tulimfanyia uchunguzi wa afya ya ubongo wake katika Hospitali ya Taifa Muhimbili hapa Dar es Salaam. Tulitumia kipimo cha CT – Scan na matokeo yameonyesha kuwa hana matatizo.

(d)Ini, Figo, Bandama, Kongosho: Mhe. Rais Kikwete kila mwaka tunapomfanyia uchunguzi wa jumla wa afya yake tumekuwa tunamfanyia kuchunguza viungo vyake muhimu vya tumboni kama vile ini, figo, bandama na kongosho. Tumekuwa tunafanya hivyo kwa kutumia kipimo cha ultra sound na kwa kupima damu yake kwa kutumia vipimo muhimu. Uchunguzi huo umebaini kuwa viungo vyote hivyo ni salama na vinafanya kazi vizuri.

(e)Mfumo wa njia ya Chakula: Mfumo mzima wa njia ya chakula (alimentary canal), yaani koromeo la chakula, tumbo, utumbo mdogo na utumbo mkubwa nao tumeufanyia uchunguzi wa kina kama kuna tatizo lolote katika kipindi cha miaka miwili hii. Mwaka 2007, tulimfanyia kipimo cha colonoscopy mjini Paris, Ufaransa, kuchunguza hali ya afya ya utumbo mkubwa. Matokeo ya uchunguzi yalionyesha kuwa utumbo wake mpana uko salama kabisa na hakuna matatizo yeyote. Daktari bingwa aliyemfanyia uchunguzi huo ameshauri kuwa Mhe. Rais hahitaji kufanya kipimo hicho tena mpaka baada ya miaka saba. Nakumbuka pia daktari huyo alimtania Mhe. Rais kuwa angefurahi kuazima utumbo wake.

Wiki mbili zilizopita, Mhe. Rais akiwa mjini New York, Marekani, alifanyiwa kipimo cha endoscopy kuchunguza kuanzia koromeo la chakula, tumbo, na utumbo mdogo. Matokeo ya uchunguzi huo yametoa majibu mazuri kuwa yako salama. Makusudio ya kufanya vipimo hivi viwili ni kuchunguza maradhi ya kansa na viashiria vya ugonjwa huo. Bahati nzuri hana maradhi hayo na wala hakuna dalili yoyote iliyoonyesha kuwapo viashiria vya kansa.

(f)Tezi la Shingo (Thyroid Glands): Aidha, wakati wa safari yake hivi karibuni majuzi mjini New York, Marekani, Mhe. Rais tulimfanyia uchunguzi wa afya ya tezi la shingo pamoja na kiwango chake cha utoaji wa homoni. Matokeo ya vipimo vyote vilivyofanyika yameonyesha kuwa hakuna matatizo yoyote.

(g)Tezi la Kibofu (Prostate): Septemba, mwaka huu, 2009, tulifanya uchunguzi wa hali ya afya ya tezi la kibofu (prostate) kwa kutumia mashine maalum na kwa kuchunguza damu yake. Vipimo vyote hivyo vimeonyesha hali si mbaya. Tezi lake lina ukubwa wa kawaida na hata vipimo vya viashiria vya kansa ya tezi hilo (PSA) tunavyofanya kwenye damu vilikuwa katika kiwango cha kawaida. Mhe. Rais hana matatizo ya prostate.

(h)Macho, Masikio na Pua: Tumeshamfanyia vipimo vya macho, masikio na pua na vyote viko salama. Mhe. Rais anavaa mawani lakini hayo si maradhi. Watu wengi baada ya kufikia umri wa miaka 40 si ajabu huhitaji mawani. Tunapofanya uchunguzi wa macho, ukiacha ile ya kuchunguza uwezo wa kuona, tunaangalia pressure ya macho na hali ya viungo vya nje na ndani ya jicho. Mhe. Rais hana matatizo yoyote.

(i)Damu: Tumekuwa tunamfanyia Mhe. Rais uchunguzi wa damu yake kwa vipimo mbalimbali vinavyotumika kutambua maradhi mbalimbali yahusuyo damu yenyewe na mwili mzima wa mwanadamu. Tumekuwa tunafanya hivyo kila baada ya miezi sita au panapojitokeza ulazima wa kufanya hivyo. Tumekuwa tunafanya hivyo hapa nchini na hata nchi za nje kwa nia ya kulinganisha matokeo yetu na kwa vipimo ambavyo sisi hatunavyo. Matokeo ya uchunguzi wetu yameonyesha kuwa Mhe. Rais yuko salama. Hana maradhi ya damu au kisukari, wala ukimwi, au ya wingi wa mafuta (cholesterol), ama ya kiwango cha madini, au ya tezi la kibofu, wala ya tezi la shingo, au ya ini, au ya homoni mbalimbali zilizoko mwilini na mengine n.k. Jambo pekee linalojitokeza ni kwamba Mhe. Rais ana damu nyingi. Hivyo, tumekuwa tunamshauri kupunguza damu kwa kuchangia Benki ya Damu. Tunashukuru amekuwa anafanya hivyo karibu kila baada ya miezi sita. Damu nyingi inaweza kuwa na madhara mwilini lakini Mhe. Rais hajafikia kiwango cha kuwa ni tatizo la kiafya. Pia tunamshukuru kwa kuwa mwepesi kukubali kupunguza damu ambayo tunaitumia kuokoa maisha ya watu wengine. Hakuna hofu yoyote.
Napenda kusema wazi watu wote wasikie na kwa ukweli kwamba mimi na daktari mwenzangu yaani Dr. Mohamed Janabi hali ya afya ya Rais silo jambo linalotutia shaka wala kutusumbua au kutunyima usingizi.

Tatizo pekee ambalo limekuwa likimsumbua Mhe. Rais mara kwa mara ni maumivu ya shingo yanayotokana na kuumia zamani utotoni na wakati wa ujana. Kuumia huko ni kwa baadhi ya pingili za uti wa mgongo, sehemu ya shingo (cervical spine), kuathirika na kumsababishia maumivu. Mara nyingi matatizo ya namna hiyo huwapata wanamichezo na wanajeshi. Kutokana na shughuli wazifanyazo. Kuumia siyo jambo la kustaajabisha.

Tutakumbuka kuwa Mhe. Rais amekuwa mwana michezo hususan mchezaji wa basketball, mpira wa miguu na hata riadha wakati wa ujana wake. Pia alikuwa mwanajeshi. Ili kutambua vizuri tatizo la shingo ili tujue namna ya kumpatia tiba tumeshamfanyia vipimo vyote muhimu vya uti wa mgongo toka juu mpaka chini. Tumetumia x-ray, CT – Scan na MRI-Scan. Pia ameshaonwa na madaktari bingwa wa upasuaji wa mishipa ya fahamu hapa nchini na nje. Pamoja na kuwepo athari katika shingo, madaktari hao kwa dhati wameshauri kuwa kwa sasa maumivu yake hayahitaji upasuaji isipokuwa mazoezi ya viungo. Mhe. Rais amefundishwa mazoezi anayotakiwa kuyafanya na amekuwa anayafanya kwa nidhamu ya hali ya juu. Matokeo yake ni kupata nafuu kubwa. Ndiyo maana siku hizo haonekani kunyoosha shingo mara kwa mara kama ilivyokuwa zamani kwa wale wanaokumbuka. Tunafuatilia kwa karibu sana hali ya shingo yake. Tunamfanyia vipimo vya MRI na kuonana na madaktari bingwa mara kwa mara.

Mwisho
Napenda kabla ya kumalizia nisisitize tena kwa kusema kuwa mimi na daktari mwenzangu hatuna mashaka na hali ya afya ya Mhe. Rais. Afya yake ni nzuri, hana maradhi yanayotishia maisha yake au kupunguza uwezo wake wa kulitumikia taifa na watu wake. Pia maoni yetu hayo ndiyo maoni ya madaktari wa ndani na wa nje waliowahi kuhusika na uchunguzi wa afya yake.

Napenda pia kuwahakikishia kuwa, sisi madaktari wake, hatutachoka kufuatilia kwa karibu na kwa umakini mwenendo wa afya ya Mhe. Rais ili tujue mapema kama kuna jambo la kushughulikia. Kwa hili lililotokea, tutaendelea kuchunguza kama jambo lolote lililojificha ambalo hatujalibaini.

Kwa sasa napenda kurudia kusema kuwa hakuna ushahidi wa kitaalamu wa kusema kuwa kulikuwa na sababu nyingine zaidi ya uchovu. Rais aliondoka New York Septemba tarehe 30 saa nane ya usiku kwa saa ya hapa Dar es Salaam kuanza safari ya kurudi nyumbani. Aliwasili nyumbani saa saba ya usiku wa tarehe 1 Oktoba. Njiani alisimama London na Nairobi kuunganisha ndege. Hivyo basi, alisafiri saa 24 bila ya kulala vizuri. Isitoshe hata kwenye ndege alitumia muda mwingi akifanya kazi. Asubuhi na mapema siku ya Oktoba 2, aliondoka Dar es Salaam kwenda Arusha kufungua mkutano wa Wabunge wa Jumuiya ya Madola saa nne asubuhi. Baadae jioni yake alishiriki kwenye hafla ya chakula cha jioni alichowaandalia wabunge. Rais aliondoka saa sita usiku kwenda kulala. Hatuna hakika alilala saa ngapi kwani najua akiwa na kazi huchelewa sana kulala. Tarehe 3 Oktoba, 2009 alikuwa na mikutano mfululizo na viongozi na wananchi pale Arusha kabla ya kuondoka majira ya alasiri kwenda Mwanza. Alipofika Mwanza alikuwa na mazungumzo na wenyeji wake usiku ule mpaka saa nne ya usiku. Tulipofuatilia tuligundua kuwa hata siku hiyo nayo alichelewa sana kulala kwani walipondoka wageni wake yeye aliendelea kushughulikia hotuba yake mpaka karibu na alfajiri. Katika mazingira hayo kupata matatizo ya mwili kuchoka sana, na hata kukataa kuendelea kutumika, na kutaka kupumzika kama ilivyotokea si jambo la ajabu.

Mwisho kabisa napenda kuwahakikishia kuwa Rais yuko salama. Afya yake ni nzuri na haina shaka yoyote. Uchovu uliokithiri ndicho chanzo cha yaliyotokea Mwanza siku ile ya tarehe 4 Oktoba, 2009. Mimi na wenzangu katika Ofisi Binafsi ya Rais (OBR) tumejifunza na tumeazimia kuwa waangalifu zaidi katika kupanga ratiba ya kazi ya Rais.

Dr. Peter Mfisi Ikulu, Dar es Salaam
Daktari wa Rais 08 Oktoba, 2009

0 feedback :

Recent Comments . Kauli za Wasomaji

###recentComment###

More Opportunities ads