wavuti.com Updates

-------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Napenda kuwataarifu kuwa blogu hii inapumzishwa rasmi na tovuti mpya imezaliwa kwa jina www.wavuti.com

This is to inform you that this blog has been retired. A new website to take her place is up and running at www.wavuti.com

Thursday, December 04, 2008

TweetThis! Watendaji, umeme wa Mbeya unapatikana wapi?

Nimesikia habari iliyonifanya nijiulize, kulikoni juu ya utendaji na utekelezaji wa haki ya kimaendeleo kwa wananchi wa Mbeya?

Inaripotiwa habari za kusikitisha ya kwamba kwa takribani wiki tatu sasa, wananchi wa Mkoa wa Mbeya wapo gizani kwa kukosekana nishati ya umeme. Simanzi zaidi ipo pale maeneo nyeti kama vile mahospitali ikiwemo ile ya rufaa ya Mbeya na sehemu nyingine za jamii, huduma ya umeme haipo. Inahuzunisha zaidi kusikia kuwa tayari vimetokea vifo ambayo vingeweza kuepukika endapo ingekuwepo nishati hiyo.

Najiuliza, mbona suala hili halizungumziwi? Mbona hakuna anayejigusa kueleza kinachoendelea na mipango ya kutengemaza hitilafu hiyo? Hadi vifo vinagapi vitokee?

Hii inasababisha wananchi wa eneo hilo waanze kufikiri kuwa wanaadhibiwa kutokana na ile kasheshe ya kurushiwa mawe msafara wa Mkuu sana wa nchi. Ingawaje inawezekana ukawepo ukweli wa kiasi cha chembe ya mchanga, bado hata kama ukweli ungekuwa unajaza kibaba kizima, visa vya kurushiwa mawe havitoshi kuwa sababu ya kuwaadhibu wananchi wa Mkoa mzima na hasa ukizingatia kuwa wanaokufa na kuteseka zaidi si ajabu hawahusiki hata kidogo na mawe hayo yaliyorushwa siku hiyo. Ikiwa hiyo ndiyo sababu ya kutokushughulikia tatizo la umeme katika mkoa wa Mbeya, basi inaonesha ni kwa kiasi gani tuna watu wasiotumia akili zao katika maamuzi yenye msingi. Ama kwa hakika, inaeshinikiza mtu kufikiri kuwa maamuzi yanayofanywa na baadhi ya viongozi wetu ni ya kibinafsi, yasiyozingatia maslahi ya Taifa na wananchi wake na yaliyojaa hasira za kipumbavu kabisa.

Mkoa wa Mbeya unatoa huduma ya afya kwa mkoa mzima na mikoa mingine inayouzunguka, hivi leo akizidiwa mgonjwa atahitaji kuhudumiwa vipi bila nguvu ya nishati ya umeme? Binadamu huyu akikosa huduma akafariki, Taifa linakuwa limepata hasara ya nguvu kazi ambayo ingawaje haiwezekani kuonekana kuwa ni jambo la kujali sana mtu mmoja akifariki, je, ni mmoja wangapi wanaofariki na jumla yao ikawa kiasi gani?

Mkoa wa Mbeya unao mchango mkubwa sana katika kukuza uchumi na kuongeza pato la Taifa kutokana na nguvu kazi za wakazi wa Mkoa huo, je, watu hawa wanapokosa nishati ya umeme, wanawezaje kuongeza ufanisi na kuboresha hali za maisha?

Ninachojali ni huu usemi kuwa 'wanalipiziwa kwa kurushia msafara wa raisi mawe'. Hii si hoja kwa sababu kwa kuwatenga na kutokuwajali, hasira yao itaongezeka mara dufu. Hufikia wakati mtu akajitoa mhanga kwa lolote pale anapopima na kugundua kuwa kuishi na kufa yote ni jibu moja, hakuna cha maana. Mtu akishayafikia maamuzi haya ni rahisi sana kujitoa mhanga na kufanya lolote bila kujali madhara yake. Ndiposa itatokea vurugu zaidi na wakiyakosa mawe, silaha za jadi zitatosha. Mishale, pinde, mikuki na manati vitatosha kutumika kama silaha. Itakuwa bora kipindi kile walichoweza kurusha mawe wakaonekana, kuliko watakapoamua kujificha na miti kisha wakatumia vijimawe vinavyotosha saizi ya kipago cha manati kulenga.

Ninyi mliobeba dhamana ya kutumikia wananchi kwa kauli zenu wenyewe muwe na heshima na mthubutu kufanya haki kila inapostahili vinginevyo, hamfai kuwa wawakilishi ama viongozi wa watu.

1 feedback :

Mzee wa Changamoto said... Thu Dec 04, 06:45:00 PM MST  

Utendaji wa nyumbani wakati mwingine ni wa kukomoana sana. Unawaweka wananchi kwenye utata wa kuuona "mstari mwembamba" kati ya Itikadi na mahitaji muhimu ya kikatiba. Yaani huduma kama Umeme inakatishwa kwa maovu ya wachache. Ama kama tulivyosikia lawama toka Pemba (ambazo siwezi kuthibitisha) kuwa walikuwa wakikosa baadhi ya huduma kwa kuwa tu walichagua upinzani. Inasikitisha na twajiuliza kama wakuu wanayaona haya ama la.
Blessings

Recent Comments . Kauli za Wasomaji

###recentComment###

More Opportunities ads