wavuti.com Updates

-------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Napenda kuwataarifu kuwa blogu hii inapumzishwa rasmi na tovuti mpya imezaliwa kwa jina www.wavuti.com

This is to inform you that this blog has been retired. A new website to take her place is up and running at www.wavuti.com

Friday, October 31, 2008

TweetThis! Hekaya II

Wakati Afrika na pengine dunia nzima ipo kimya kusubiri kuona matokeo ya uchaguzi wa uraisi wa Marekani yatakuwa vipi, mtu mmoja ambaye nimekuwa nikifuatilia kwa karibu sana maendeleo na jitihada za kuikwamua nchi yake kimaendeleo anafanya yote anayoweza kufanya kwa juhudi na maarifa.

Majuzi, wakati sisi Tanzania tunabishana juu ya habari za uchaguzi mdogo huku waalimu wakitaabika na halali za malipo yao, mtu huyu ametangaza kusaini na kuanza utaratibu wa kupatikana kwa kompyuta za bei nafuu kwa kila mtoto katika nchi yake. Mheshimiwa huyu amekuwa akitizama zaidi juu ya mustakabali wa Taifa lake, wachilia mbali kama sera za chama chake zinapishana na mipango endelevu ya Taifa lake. Uamuzi wake wa kuacha mambo ya chama yajishughulikie yenyewe na utaifa kwanza usonge mbele umenivutia kuifahamu siri aliyonayo huyu. Nimemsikia akisemwa vibaya kuhusiana na 'kuwasaidia waasi wa Kongo DRC' lakini kama vile hizo ni kelele za vyura mtoni zisizomzuia Tembo kunywa maji, yeye amezidi kusiriba mdomo wake kwa ukimya na kuimarisha si tu jeshi lake bali na ulinzi wa mipaka ya nchi yake. Mwenzetu huyu katoka kwenye vita, anaifahamu fika shubiri ya kifo na gharama zilizowapata kama Taifa katika vita ile na yupo tayari kulipanga jeshi.

Huyu kaishangaza dunia wiki chache zilizopita alipofutilia mbali matumizi ya lugha ya Kifaransa kama lugha ya utambulisho wa Taifa na kama vile haitoshi, kaamuru itumike mashuleni kama lugha rasmi na zingine zifuate. Kajifunza siri gani huyu kuwa lugha ya biashara, kisomo na maendeleo ni Kiingereza? Wakati WaTanzania tunaimba juu ya vita ya Kagera ya mwaka 1977, mwenzetu huyu akitusikia sijui atatudhania wehu na majuha wa sayari gani vile! Vile alinganishe na yaliyotukia nchini mwake mwaka 1994, yaani anapatwa na butwaa! Hivi sasa bwana huyu, kusema hasemi sana kauli yake kitendo tu, na kwa kweli kauli isiyoambatana na kitendo si mali kitu. Maneno huzungumza kirefu na cha kudumu zaidi ya maneno matupu yasiyovunja ama kuganga mfupa. Amefahamu fika kuwa siri ya maendeleo ni kujiunga katika Jumuiya, kutumia lugha iliyotapakaa kotekote na kuachana na kasumba ya ukoloni na historia isiyofaa chochote! Ikiwa koloni lake kihistoria lingekuwa la manufaa basi mauaji ya kimbari yaliyotukia mwaka ule yasingethubutu kukaribia hata robo ya kiwango kilichotukia. Hata ingelikuwa ni ndani ya maamuzi yangu, ningesafisha na kuondoa kabisa kila aina ya takataka niliyorithi kwa wazazi na mababu ikiwa yote ninayopata kwayo ni maudhi, hasara na mauti.

Safari zake mheshimiwa huyu za mahesabu na mipango.
Lugha yake huyu hawaielewi majirani viongozi wenzie kwani mbalimbali fumbo zake zimefumbika. Kila anaposema japo anautaja ukweli peupe, wenziwe wanaziona kama tamathali za semi na mara wanapotahamaki, yailani amepiga hatua tatu mbele. Walimu na Wakufunzi wetu anao. Wafanya kazi bora na makini toka kwetu ndiyo watendaji kazi wake. Wasomi wazawa wa nchi yake, wamesomea kwenye vyuo vyetu na wengine wamekutana na WaTanzania katika vyuo vya ng'ambo, sasa iweje wao wakarejea na kuchagiza maendeleo kwao sisi tunafichiana kamba za viatu?

Sawa! Nakubali. Kwamba sisi WaTanzania tumebarikiwa sana na tunamshukuru aliyetugawia Mlima Kilimanjaro, madini ya Tanzanite, Almasi na Dhahabu, mbuga za Wanyama tena moja ya hizo ikawa ndiyo kubwa kuliko zote zilizoonekana hapa Duniani, maji kila pembe ya mpaka wa nchi toka Mashariki ilipo Bahari ya Hindi hadi Magharib kwenye Ziwa lenye kina kirefu Tanganyika, toka Kaskazini tulipogawiwa sehemu kubwa kuliko nchi zote zinazoshiriki Ziwa Victoria hadi Kusini penye mchirizi wa sehemu ziwa Malawi. Ninayo nafasi ya kutaja Duluti, Eyasi, Rukwa na bonde la Malagarasi bila kusahau mito isiyochoka kumwaga machozi Pangani, Ruvu, Wami, Kagera na Ruvuma. Nitakuwa sikupita darasa la tatu ikiwa nitasahau Historia ya fuvu la mtu wa kale Duniani liligundulika Olduvai wachilia mbali historia za Bagamoyo, Amboni, Irangi, Isimani na Kalenga. 'Aliyetupa siye kiti ndiye aliwapa wao kumbi'. Nikilinganisha haya machache na utajiri wa nguvu kazi ya watu na jirani zetu hawa walivyo na rasilimali haba na uchache wa raia, hivi kwa hakika hatakosea Paul Kagame ataposema, 'penye miti hakuna wajenzi' nasi tukamgeuza, 'cha mlevi huliwa na mgema'.

Sawa na kucheza mpira wa miguu.
Unajua, mchezo wa mpira wa miguu unavutia inapoundwa timu. Na kila timu inaye golikipa na wachezaji. Kiwanjanii lazima pia wawepo wanachama, mashabiki na watazamaji, na bila shaka lazima uwepo uwanja, mpira, refarii na washika vibendera.
Sasa wewe uwe katika mechi hiyo. Golikipa afahamu kuwa raha ya kuwepo mpirani ni mpira wenyewe na kwamba ukikosekana huo, basi hautakuwa mpira wa miguu tena huo bali uwanja wa gumzo na pengine magumi haswa patashika nguo kuchanika. Sasa fikiri golikipa aukumbatie mpira, wachezaji wajitahidi kumnyang'anya naye aufukie ndani ya jezi yake ama aketi chini aufichame chini ya magoti! Patakalika hapo? Mbata atakazopata huyo, uchungu wa maumivu yake ni afadhali ya kulishwa mchunga mbichi.
Sasa fikiri kuwa katika kuuficha mpira huo, aliudondosha kwa bahati mbaya mchezaji wa timu pinzani akaubetua kimoja hadi golini....! Vipi, ndiyo bao tayari tena hilo.

Basi ndivyo tulivyo Tanzania.
Tumepigwa bao kwa kuficha mpira na tukaudondosha kwa bahati mbaya wakaubetua waliokuwa wakiumezea mate.
Tumekalia yoooote tuliyobarikiwa kupewa katika nchi yetu. Tumebana weeeee, mwishowe tumeachia kiduchu tu, salale!, kumbe wapo wanjanja wamegundua mpira ulipo. Ni magoli tunafungwa tu kila tunapogeuka. Tumeanza kunyoosheana vidole, tunaambizana kwa jazba, tunabishana pasina sababu kwa mambo ambayo yatatuongezea mtafaruku tu. Tumebakiza kushikana mashati tu, na ama kwa hakika unafahamu kitakachofuata baada ya mtu kumkwida mwenziwe shati. Madhara yake hapo, walijisemea wahenga, 'majuto ni mjukuu' na 'maji yakishamwagika hayazoleki'. Tusije utumbua usaha na kujenga donda ndugu! Tafadhali tena chondechonde! Hakuna faida hata ya uzito usawa wa chembe moja ya mchele katika magomvi.

Nasemaje, niwache nitoke kwanza kidogo naona Kagame yulee, nataka ntizame anakouelekeza mguu...

0 feedback :

Recent Comments . Kauli za Wasomaji

###recentComment###

More Opportunities ads